MAKATIBU WAKUU WAKUTANA KUJADILI UCHUMI WA BULUU ZANZIBAR.

Imewekwa: Thursday 13, April 2023

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (SMT) Prof. Riziki Shemdoe pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi (SMZ), Dkt. Aboud Jumbe jana tarehe 6 machi 2023, wamekutana Mjini Zanzibar katika Ofisi za WUBU kujadili suala la kuimarisha uchumi wa Buluu.

Aidha, majadiliano hayo yalijikita katika kuangalia namna bora ya kufanya tathmini ya wingi na mtawanyiko wa samaki kwenye ukanda wa uchumi wa bahari ili kuvutia uwekezaji mkubwa zaidi katika uvuvi wa bahari kuu.

Makatibu Wakuu hao wakiwa pamoja na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bara Bi. Agnes Meena pamoja na maafisa kadhaa wa pande zote mbili yaani Bara na Zanzibar wamejadiliana kwa kina namna ambayo uchumi wa buluu utawezesha Serikali hizi kunufaika zaidi na rasilimali za uvuvi.

Vilevile, katika majadiliano hayo baadhi ya taasisi zilizochini ya Wizara hizo mbili zilishiriki katika majadikiano hayo ikiwemo TAFIRI, ZAFIRI, Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu (DSFA) pamoja na Maafisa Uvuvi, wanasheria na Watafiti.

Aidha, kikao hicho kilihitimishwa kwa kukubaliana masuala kadhaa ikiwemo kuboresha mashirikiano kati ya taasisi za utafiti za TAFIRI na ZAFIRI, kufungua Milango ya ushirikiano kati ya taasisi hizo za utafiti na Sekta binafsi katika kufanya tathmini hiyo.

Halikadhalika, Viongozi hao walikubaliana ushiriki wa Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu ili kuwa na taarifa zitakazowasaidia kutoa maamuzi ya kiasi gani cha uvuvi hasa wa Dagaa na aina zingine za samaki wadogo wanaopatikana katika tabaka la juu.

Awali Makatibu Wakuu hao wamewashukuru Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Dkt. Husein Mwinyi,Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kwa kuweka nguvu kubwa kwenye kuhakikisha nchi yetu inanufaika zaidi na rasilimali za uvuvi katika ukanda wa uchumi wa bahari.

.